Saturday, December 13, 2025

CHALAMILA AITAKA DAWASA KUBUNI SULUHISHO LA KUDUMU KUKABILIANA NA UPUNGUFU WA MAJI MT0 RUVU










Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, ameitaka Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kuweka mikakati madhubuti na ya kudumu ya kukabiliana na changamoto ya upungufu wa maji katika vyanzo vya maji, hususan Mto Ruvu, unaojitokeza mara kwa mara katika vipindi virefu vya ukosefu wa mvua.

Akizungumza kuhusu hali ya upatikanaji wa majisafi jijini Dar es Salaam, Mhe. Chalamila amesema changamoto ya upungufu wa maji katika Mto Ruvu si jambo jipya, hivyo kuna umuhimu mkubwa kwa watendaji na wataalamu wa sekta ya maji kukaa pamoja na kubuni suluhisho la muda mrefu litakalosaidia kuondokana na athari zinazowakumba wananchi kila inapotokea hali ya ukame.

Amesisitiza kuwa DAWASA inapaswa kubuni na kutekeleza miradi ya maji itakayowezesha upatikanaji wa huduma ya maji kwa uhakika hata katika vipindi vya upungufu wa maji, ili kukidhi mahitaji ya wananchi wa Jiji la Dar es Salaam linaloendelea kukua kwa kasi.

“Kwa kuwa changamoto hii inajirudia mara kwa mara, ni wajibu wa DAWASA kuhakikisha inabuni miradi ya kimkakati itakayowezesha upatikanaji wa majisafi kwa kipindi chote cha uhaba wa maji, hususan wakati wa kiangazi,” amesema Mhe. Chalamila.

Aidha, Mkuu wa Mkoa ameitaka DAWASA kuongeza jitihada katika kufufua visima vya maji vilivyopo ili viweze kutoa huduma ipasavyo, hatua itakayosaidia kupunguza malalamiko ya wananchi kuhusu upungufu wa maji katika maeneo mbalimbali ya jiji.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa DAWASA, Mhandisi Romanus Mwangingo, amesema mamlaka hiyo imepokea maelekezo yote yaliyotolewa na Mkuu wa Mkoa na tayari hatua zinaendelea kuchukuliwa ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji kwa haki na usawa.

Mhandisi Mwangingo ameongeza kuwa DAWASA inaendelea na jitihada za kutoa maji kwa mgao sawia katika maeneo yote ya jiji, sambamba na kufufua visima vilivyopo kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa majisafi na kupunguza athari za uhaba wa maji kwa wananchi.

Naye Mkurugenzi wa Bonde la Wami Ruvu, Mhandisi Elibariki Mmasi, amesema changamoto ya upungufu wa maji katika Mto Ruvu imesababishwa kwa kiasi kikubwa na athari za mabadiliko ya tabianchi, ambazo zimeendelea kuathiri vyanzo vya maji katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Ameeleza kuwa hatua kadhaa tayari zimechukuliwa, ikiwemo kusitisha utoaji wa vibali kwa watumiaji wa skimu za umwagiliaji katika kipindi cha kiangazi, kwa lengo la kulinda na kuimarisha wingi wa maji katika vyanzo vya maji, hususan Mto Ruvu.

Hatua hizo zinatarajiwa kusaidia kupunguza makali ya uhaba wa majisafi na kuhakikisha huduma ya maji inaendelea kupatikana kwa wananchi wa Jiji la Dar es Salaam, huku Serikali ikiendelea kusisitiza suluhisho la kudumu kwa changamoto ya maji.

DKT. JAKAYA KIKWETE AAGA MWILI WA JENISTA MHAGAMA DODOMA

Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, akiwasili katika Kanisa Katoliki la Mwenyeheri Maria-Theresa Ledochowska, Parokia ya Kiwanja cha Ndege, Jijini Dodoma, kushiriki ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Marehemu Jenista Joakim Mhagama leo, tarehe 13 Desemba, 2025



 

RAIS SAMIA: JENISTA MHAGAMA ALITANGULIZA MASLAHI YA TAIFA, ALIKUWA NGUZO YA MATUMAINI KWA WENGI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akizungumza na waombolezaji mara baada ya ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Marehemu Jenista Joakim Mhagama, katika Kanisa Katoliki Parokia ya Kiwanja cha Ndege, Jimbo Kuu la Dodoma, tarehe 13 Desemba, 2025
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiongoza waombolezaji kuaga mwili wa aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Marehemu Jenista Joakim Mhagama, katika ibada iliyofanyika katika Kanisa Katoliki Parokia ya Kiwanja cha Ndege, Jimbo Kuu la Dodoma, tarehe 13 Desemba 2025.


Picha za matukio mbalimbali wakati wa ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Marehemu Jenista Joakim Mhagama katika Kanisa Katoliki Parokia ya Kiwanja cha Ndege, Jimbo Kuu la Dodoma, tarehe 13 Desemba, 2025.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Marehemu Jenista Joakim Mhagama alikuwa kiongozi aliyeitanguliza mbele maslahi ya Taifa kabla ya kitu kingine chochote, akibainisha kuwa sehemu ya uimara na mafanikio ya Taifa yalichangiwa kwa kiasi kikubwa na uchapakazi na uadilifu wake.

Rais Samia ameyasema hayo wakati wa ibada ya kuaga mwili wa Marehemu Jenista Mhagama iliyofanyika katika Kanisa Katoliki Parokia ya Kiwanja cha Ndege, Jimbo Kuu la Dodoma, tarehe 13 Desemba 2025. Ibada hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, viongozi wa Bunge, viongozi wa dini pamoja na mamia ya wananchi waliokusanyika kutoa heshima zao za mwisho kwa marehemu.

Akizungumza mbele ya waombolezaji, Rais Samia amesema Mhe. Jenista Mhagama alipendwa na kuheshimiwa sana na watu wote, hususan waliokuwa chini ya uongozi wake, kutokana na utendaji wake uliotukuka na moyo wa kujitoa kwa ajili ya nchi. Rais ameeleza kuwa alimpa jina la “kiraka” kwa sababu kila sehemu alipowekwa aliitumikia kwa ufanisi, uaminifu na matokeo chanya.

Aidha, Rais Samia amesema mafanikio ya Bunge na Taifa kwa ujumla yanategemea mshikamano wa viongozi wote wakiwemo Wabunge na Mawaziri, bila kujali tofauti zao. Amesisitiza kuwa Mhe. Jenista Mhagama alikuwa kiongozi jasiri, mlezi wa wengi ndani ya Bunge na Serikali, na nguzo ya matumaini kwa wanawake na vijana, akiongozwa na nidhamu ya hali ya juu katika utendaji wake.

Kwa upande wake, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi, amesema Marehemu Jenista Mhagama alikuwa mtumishi wa kweli wa wananchi, mnyenyekevu na mwenye mapenzi ya dhati kwa watu wake. Makamu wa Rais amesema katika maisha yake ya utumishi, jambo alilolitanguliza zaidi ni kuwatumikia wananchi wa Jimbo la Peramiho kwa moyo wote.

Makamu wa Rais ameongeza kuwa kama angepewa nafasi ya kuomba jambo moja kwa Mwenyezi Mungu, angeomba viongozi wote—Wabunge na Madiwani—wapende na kuwahudumia wananchi wao kwa kiwango cha kujitolea na uadilifu alioonyesha Marehemu Jenista Mhagama.

Naye Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Azzan Zungu, ametoa pole kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, familia ya marehemu, Wabunge na Watanzania kwa ujumla, kwa kuondokewa na kiongozi mahiri aliyeipenda nchi yake kwa dhati. Spika amesema Marehemu Mhagama alikuwa mtu aliyekuwa mnyenyekevu, aliyejishusha na kuwaheshimu watu wote bila kujali nafasi zao.

Akizungumza kwa niaba ya familia, mtoto wa Marehemu Jenista Mhagama, Victor Mhagama, amesema mama yao aliwafundisha kupenda kazi, kuwa na uzalendo wa kweli na kumcha Mungu. Amesema marehemu aliwausia kuchapa kazi kwa bidii, kujali utu wa watu wote na kusimamia haki bila upendeleo.

Victor ameongeza kuwa marehemu hakubagua watu kwa misingi ya hadhi, mali au umri, bali aliwahudumia wote kwa upendo na haki, akibaki kuwa kiongozi wa maendeleo na mwenye mapenzi makubwa kwa wananchi wa Peramiho na Taifa kwa ujumla.

Mwili wa Marehemu Jenista Joakim Mhagama unatarajiwa kuzikwa tarehe 16 Desemba 2025 katika Kijiji cha Ruanda, Wilaya ya Mbinga, ambako ndiko atakapopumzishwa katika nyumba yake ya milele.

#JenistaMhagama #RIPJenistaMhagama #RaisSamia #UongoziWaHuduma #TaifaKwanza #Peramiho
#Dodoma #Tanzania

Thursday, December 11, 2025

Makamu wa Rais Aongoza Salamu za Rambirambi kwa Kifo cha Jenista Mhagama, Ataja Taifa Kupata Pengo Kubwa

 










#RIPJenistaMhagama #Tanzania #Ruvuma #Uongozi

Dodoma – Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amesema taifa limepata pengo kubwa kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Peramiho na kiongozi mashuhuri wa muda mrefu, marehemu Jenista Mhagama.

Akitoa salamu za rambirambi nyumbani kwa familia ya marehemu katika eneo la Itega jijini Dodoma, Makamu wa Rais amesema Jenista Mhagama alikuwa kiongozi shupavu, mwenye heshima na mchango mkubwa katika utumishi wa umma, si tu kama Mbunge wa Peramiho bali pia kama mtendaji aliyeisimamia kwa karibu maendeleo ya Mkoa wa Ruvuma na majukumu mbalimbali ya kitaifa.

Amesisitiza kuwa marehemu Mhagama alitoa mchango mkubwa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na katika nafasi zote alizowahi kushika, akionesha uadilifu, nidhamu na uzalendo uliotukuka.

Makamu wa Rais ametumia fursa hiyo kufikisha pole kwa familia, ndugu na waombolezaji wote, akiwaombea faraja na ujasiri wa kuendelea mbele katika kipindi hiki kigumu. Amesema kifo ni sehemu ya safari ya mwanadamu, lakini alama na mchango wa marehemu Mhagama vitaendelea kukumbukwa.


#RIPJenistaMhagama #MakamuWaRais #Dodoma #Peramiho #Ruvuma #CCM #Tanzania

Wednesday, December 10, 2025

Slovakia Yafungua Ubalozi Tanzania







Balozi Mteule wa kwanza wa Slovakia nchini Tanzania, Mhe. Ivan Lančarič amewasilisha Nakala za Hati za Utambulisho kwa Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Ngwaru Maghembe jijini Dodoma Desemba 10, 2025. 

Mhe. Lančarič amewasilisha Nakala hizo za Hati za Utambulisho kufuatia nchi yake kufungua Ubalozi nchini Mwezi Desemba 2025. 

Akipokea Nakala za Hati hizo, Mhe. Maghembe amesema ufunguzi wa Ubalozi huo ni matokeo ya utekelezaji uliotukuka wa Diplomasia ya Tanzania duniani, chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan. 

"Ubalozi huu utakuwa kichocheo cha kukuza ushirikiano wa kidiplomasia baina ya Tanzania na Slovakia, hususan katika nyanja za uwekezaji, biashara na utalii", Dkt. Maghembe alisema.

Kwa upande wake, Mhe. Lančarič alieleza ufunguzi wa ubalozi mpya nchini Tanzania ni utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje ya nchi hiyo, ambayo inalenga kutanua wigo wa uwakilishi barani Afrika. Alisema Ubalozi huo utawakilisha sio tu Tanzania bali nchi nyingine za Afrika kama vile Zambia, Malawi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Congo Brazzaville, Burundi, Gabon, Cameroon na Guinea ya Ikweta

Monday, December 08, 2025

HESLB NA ADAPT IT ZAINGIA MAKUBALIANO RASMI









Dar es Salaam, Jumatatu, Disemba 08, 2025

Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imeingia katika hatua nyingine ya mageuzi ya kidijitali baada ya kuingia makubaliano rasmi na kampuni ya kimataifa ya TEHAMA, ADAPT IT ya Afrika Kusini, yenye uzoefu mpana katika kuendeleza mifumo ya elimu na fedha barani Afrika. 

Hafla fupi ya utiaji saini wa makubaliano hayo imefanyika leo, tarehe 8 Desemba, 2025 katika ofisi za HESLB kanda ya pwani, zilizopo jijini Dar es Salaam, na kuhudhuriwa na viongozi kutoka pande zote mbili.

Makubaliano hayo yanalenga kuimarisha mfumo wa usimamizi wa mikopo ya elimu ya juu ili kuongeza ufanisi, uwazi na usalama wa taarifa. HESLB kwa miaka kadhaa imekuwa ikitekeleza mageuzi ya kidijitali ili kukabiliana na ongezeko la wanafunzi wanaoomba mikopo, mahitaji ya uwazi wa taarifa na kuimarisha mifumo ya urejeshwaji mikopo kwa wahitimu.

Kupitia ushirikiano huu, ADAPT IT itasaidia HESLB kuboresha mifumo ya kiteknolojia, kuboresha mifumo mipya inayowezesha urahisi wa kupata taarifa na kuboresha miundombinu ya usalama wa data. Hii ni hatua muhimu katika kulinda taarifa nyeti za wanafunzi na wahitimu, sambamba na kuboresha kasi ya utoaji huduma bora.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Dkt. Bill Kiwia amesisitiza kuwa uhusiano huo ni sehemu ya mkakati wa Bodi katika kuhakikisha huduma za mikopo zinatolewa kwa ufanisi zaidi, kwa kuzingatia kuwa ADAPT IT wana uzoefu mkubwa katika elimu ya juu wa kutoa huduma kwa nchi zaidi ya 41 duniani.

 “Tunaamini kwamba teknolojia ni msingi wa utoaji huduma bora... Ushirikiano huu na ADAPT IT utatuongezea uwezo wa kuhakikisha tunatoa huduma bora na kwa wakati, kupitia kufanya maboresho ya mifumo yetu kuwa ya kisasa zaidi, salama na rafiki kwa watumiaji”, amesema Dkt. Kiwia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji ADAPT IT Bw. Luxolo Rubushe, amesema kuwa wako tayari kutoa utaalamu, uzoefu na ubunifu utakaowezesha HESLB kupata mifumo yenye viwango vya kimataifa. “Tunashirikiana na vyuo mbalimbali katika nchi kama Kenya, Rwanda, Afrika Kusini, Namibia, Lesotho, Botswana, Ghana na nyingine nyingi ndani na nje ya bara la Afrika. 

Tupo tayari kushirikiana na HESLB kuleta mageuzi chanya kwa kutumia teknolojia. Ushirikiano wetu na HESLB ni fursa ya kushirikiana katika kuboresha huduma za mikopo ya elimu ya juu inayotolewa na kusimamiwa nchini Tanzania,” amesema Bw. Rubushe.

Makubaliano hayo yanajikita katika maeneo muhimu yafuatayo:

* Kukuza ushirikiano kati ya HESLB na ADAPT IT kupitia majukwaa ya kidijitali kwa ajili ya kuimarisha usimamizi wa mikopo ya wanafunzi na uzingatiaji wa taratibu.

* Kutambua na kutekeleza shughuli za pamoja kama vile kampeni za uhamasishaji, suluhisho za kiteknolojia na kujenga uwezo kwa watumishi, na

* Kujifunza kuhusu fursa za ADAPT IT katika kupata suluhisho za teknolojia na kusaidia ajenda ya HESLB ya mageuzi ya kidijitali.

Kupitia makubaliano haya, HESLB inatarajia kuongeza ufanisi wa utoaji mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu, kuongeza kiwango cha makusanyo ya mikopo na kupunguza changamoto zinazotokana na ucheleweshaji wa taarifa au mifumo kukwama. Wanufaika wa mikopo, waajiri na wadau wengine pia watanufaika na mifumo iliyoboreshwa ambayo itawapa uwezo wa kufuatilia taarifa muhimu kwa urahisi.

Makubaliano kati ya HESLB na ADAPT IT ni hatua muhimu katika safari ya mageuzi ya kidijitali ndani ya sekta ya elimu ya juu nchini Tanzania. Ni hatua inayodhihirisha dhamira ya serikali katika kutumia teknolojia kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi na kuhakikisha rasilimali za umma zinasimamiwa kwa ufanisi.

KAMPUNI YA NOBLE HELIUM KUTOA AJIRA MPYA 50 KUPITIA UTAFITI WA HELIUM KINAMBO




Rukwa

Kampuni ya Noble Helium kutoka Australia imetangaza mpango wa kuajiri zaidi ya vijana 50 kupitia utafiti mpya wa Helium unaotarajiwa kuanza mwezi Desemba hadi Februari katika kijiji cha Kinambo, Wilayani Sumbawanga mkoani Rukwa.

Akizungumza kupitia mahojiano maalum hivi karibuni Mwakilishi wa Kampuni hiyo, Pius Simeon Mwita, alisema Noble Helium imefanikisha tafiti mbalimbali za awali na kubaini viashiria muhimu vya uwepo wa gesi ya Helium, huku ikichangia ajira na maendeleo kwa jamii zinazozunguka maeneo ya uchimbaji.

Mwita alisema katika tafiti zilizopita kampuni ilitoa ajira zisizo rasmi zipatazo 450, na pia ilishirikisha wananchi kwenye utoaji wa huduma kama ulinzi, usambazaji wa bidhaa, vilainishi kwa shughuli za uchorongaji, zabuni ndogo, ununuzi wa chakula pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya barabara.

Aidha, alisema Noble Helium imekamilisha tathmini na ulipaji wa fidia kwa wananchi waliopo katika maeneo ya leseni ya utafiti wa Helium, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha shughuli za kampuni zinaendeshwa kwa kuzingatia maslahi ya jamii na sheria za nchi.

Kwa mujibu wa Mwita, utafiti mpya utakaofanyika Kinambo utaongeza nafasi nyingine zaidi 50 kwa vijana, na hivyo kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika eneo hilo. 

“Tunawaomba vijana wajitokeze kwa wingi pindi fursa hizi zitakapotangazwa. Lengo letu ni kuhakikisha jamii inanufaika moja kwa moja na uwekezaji huu,” alisema.

Utafiti huo unatarajiwa kuongeza kasi ya maandalizi ya uwekezaji mkubwa wa Helium nchini, gesi ambayo imekuwa na mahitaji makubwa duniani kwa matumizi ya teknolojia za tiba, anga na vifaa vya sayansi.

CHALAMILA AITAKA DAWASA KUBUNI SULUHISHO LA KUDUMU KUKABILIANA NA UPUNGUFU WA MAJI MT0 RUVU

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, ameitaka Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kuweka mikak...